Na kila mnacho kitoa, ikiwa kwa kheri au shari, au mnacho lazimika kutoa kwa ut'iifu, basi Mwenyezi Mungu anakijua na atakulipeni. Na wale wenye kudhulumu, wanao toa kwa ajili ya kujionyesha kwa watu au wale wanapo toa wanawaudhi masikini za Mungu, au wanao toa kwa ajili ya maasi, hawatakuwa na watu wa kuwanusuru na adhabu ya Mwenyezi Mungu huko Akhera.
Na ikiwa mtazidhihirisha sadaka zenu, bila ya makusudio ya kutaka kujionyesha kwa watu, ni vizuri kwenu, inapendeza, na kwa Mola wenu Mlezi inasifika. Na pindi mkiwapa mafakiri kwa siri ili msiwatie haya, na kwa kuogopa riya (kujionyesha), basi nayo ni kheri kwenu. Na Mwenyezi Mungu atakusameheni dhambi zenu kwa sababu ya usafi wa niya zenu katika kutoa sadaka zenu. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayo yaficha na mnayo yadhihirisha, na anazijua niya zenu mnapo dhihirisha na mnapo ficha.
Si juu yako wewe, ewe Muhammad, kuwaongoa hao walio potea au kuwalazimisha watende kheri. Lilio juu yako ni kufikisha ujumbe tu. Na Mwenyezi Mungu humwongoa amtakaye. Na msaada wowote mnao toa kumpa mtu, faida yake inarejea kwenu wenyewe. Mwenyezi Mungu atakulipeni kwayo. Haya ni hivyo ikiwa mnapo toa hamkusudii ila kumridhi Mwenyezi Mungu. Na kheri yoyote mnayo itoa kwa njia hii itarejea kwenu, na mtazipata thawabu zake kwa ukamilifu bila ya kudhulumiwa chochote.
Na kutoa huko ni kwa kuwapa mafakiri ambao kwa sababu ya kuwania jihadi hawawezi kujichumia wenyewe, au ambao kwa sababu ya kuumia katika jihadi wameemewa na kuweza kuhangaika katika nchi kutafuta riziki. Na juu ya hivyo wanajizuia na kuomba omba. Asiye wajua huwadhania kuwa ni matajiri, lakini wewe utajua hali yao kwa alama zake. Na kila mtacho kitoa kwa wema, basi Mwenyezi Mungu anakijua, naye atakulipeni malipo ya kutosha.
Wale ambao dasturi yao ni kutoa kwa ukarimu wa nafsi zao usiku na mchana, mbele za watu na katika siri, watapata malipo yao kutokana na Mola wao Mlezi. Hawatofikiwa na khofu yoyote baadae, wala hawatakuwa na huzuni kwa kukosa chochote.