Mkisibiwa na madhara na mkakabiliwa na khatari katika bahari, hukukimbieni wote hao muwaombao kwa haja zenu isipo kuwa Mwenyezi Mungu peke yake. Kwani nyinyi hapo hamumkumbuki mwenginewe. Lakini akisha kuvueni na kuzama na akakufikisheni nchi kavu, mnaacha Tawhid, kumuabudu Mwenyezi Mungu Mmoja, na mnakufuru neema. Ndio mtindo wa binaadamu daima kukataa neema.
Na hapo tukisha kuvueni mkafika nchi kavu, kwani ndio mmeaminisha kuwa basi haikupateni adhabu ya Mwenyezi Mungu? Hasha! Akitaka anaweza akaipindua ardhi ikakuteketezeni chini yake. Na akitaka atakupelekeeni upepo mkali ukutupieni kokoto na mawe, na wala msipate wa kukulindeni na yanayo kupateni.
Au nyinyi mmeaminisha kuwa Mola wenu Mlezi hatakurejesheni tena baharini, na akuleteeni tufani la upepo livunjilie mbali hicho chombo chenu? Akakuzamisheni kwa sababu ya kuto thamini neema yake pale alipo kuokoeni mara ya kwanza? Tena hapo hamtapata wa kukuteteeni kwetu kwa tuliyo kufanyieni ili mpate kusalimika.
Na hakika Sisi tumewatukuza wana wa Adam kwa kuwapa umbo zuri lilio nyooka, na matamshi, na uwezo wa kukhiari mambo. Na tukawapa hishima na utukufu pindi wakit'ii. Na tukawapakia nchi kavu juu ya wanyama, na baharini katika marikebu, na tukawaruzuku vitu vitamu, na tukawafadhilisha fadhila kubwa kuliko viumbe vingi kwa kuwapa akili na kuweza kufikiri.
Ewe Nabii! Waambie watu wako: Siku tutapo waita kila kikundi kwa alama zao wanazo zijua, au mwongozi wao wanaye mfuata, au Nabii, au Kitabu wakaambiwa: Enyi watu wa Musa! Au Enyi watu wa Qur'ani! Na kadhaalika, ili wapokee vitabu vya a'mali zao. Basi atakaye pokea kitabu cha a'mali zake kwa mkono wake wa kulia, na hao ndio wenye bahati njema, hao watasoma kitabu chao kwa furaha. Na wala hawatapunguziwa katika ujira wao duni ya kitu.
Ama yule wa kikundi kingine yatamhuzunisha atayo yaona. Na atazibiwa njia za kuokoka. Na atakuwa kipofu asione pa kuepuka adhabu yake, kama alivyo kuwa duniani kipofu haioni Njia ya Haki na Uwongofu! Na anaye kuwa duniani kipofu (wa moyo) basi Akhera ni kipofu zaidi, na yu mbali zaidi na Njia ya Kheri.
Hakika washirikina wanatafuta kila njia wakuachishe Qur'ani utafute miujiza myengineyo, ili uwe kama uliye tuzulia Sisi uwongo. Na hapo ndio watakufanya uwe rafiki yao! Na hila hizi zimekaririwa na zimekuwa nyingi. Na kwa hivyo ungeli karibia kuyafuata wayatakayo, ila kwa kuwa wewe ni Mtume wetu uliye muaminifu, hayakuwa hayo.
Upole wetu umekugubika wewe, tukakulinda usiwakubalie matakwa yao, na tukakupa nguvu usimame juu ya Haki. Na lau kuwa si hayo ungeli karibia kuwakubalia kwa tamaa ya kuwa huenda ikafika siku imani yao ikakamilika baadae wakisha anza kuingia katika Uislamu.
Na lau ungeli karibia kuwaelekea hao, basi tungeli kukusanyia adhabu za duniani tukazifanya mardufu, na adhabu za Akhera nazo tukaziongeza mara mbili vile vile. Na wala usingeli pata yeyote wa kukunusuru na adhabu. Lakini hayo hayawi kabisa, hayawezi kumfikilia Mtume wetu Muaminifu.