કુરઆન મજીદના શબ્દોનું ભાષાંતર - સ્વાહિલી ભાષામાં અનુવાદ - અલી મોહસીન અલ્ બર્વાની

પેજ નંબર:close

external-link copy
12 : 4

۞ وَلَكُمۡ نِصۡفُ مَا تَرَكَ أَزۡوَٰجُكُمۡ إِن لَّمۡ يَكُن لَّهُنَّ وَلَدٞۚ فَإِن كَانَ لَهُنَّ وَلَدٞ فَلَكُمُ ٱلرُّبُعُ مِمَّا تَرَكۡنَۚ مِنۢ بَعۡدِ وَصِيَّةٖ يُوصِينَ بِهَآ أَوۡ دَيۡنٖۚ وَلَهُنَّ ٱلرُّبُعُ مِمَّا تَرَكۡتُمۡ إِن لَّمۡ يَكُن لَّكُمۡ وَلَدٞۚ فَإِن كَانَ لَكُمۡ وَلَدٞ فَلَهُنَّ ٱلثُّمُنُ مِمَّا تَرَكۡتُمۚ مِّنۢ بَعۡدِ وَصِيَّةٖ تُوصُونَ بِهَآ أَوۡ دَيۡنٖۗ وَإِن كَانَ رَجُلٞ يُورَثُ كَلَٰلَةً أَوِ ٱمۡرَأَةٞ وَلَهُۥٓ أَخٌ أَوۡ أُخۡتٞ فَلِكُلِّ وَٰحِدٖ مِّنۡهُمَا ٱلسُّدُسُۚ فَإِن كَانُوٓاْ أَكۡثَرَ مِن ذَٰلِكَ فَهُمۡ شُرَكَآءُ فِي ٱلثُّلُثِۚ مِنۢ بَعۡدِ وَصِيَّةٖ يُوصَىٰ بِهَآ أَوۡ دَيۡنٍ غَيۡرَ مُضَآرّٖۚ وَصِيَّةٗ مِّنَ ٱللَّهِۗ وَٱللَّهُ عَلِيمٌ حَلِيمٞ

Na fungu lenu ni nusu walicho acha wake zenu ikiwa hawana mtoto. Wakiwa na mtoto basi fungu lenu ni robo ya walicho acha, baada ya wasia waliyo usia au kulipa deni. Na wake zenu watapata robo mlicho kiacha, ikiwa hamna mtoto. Mkiwa mna mtoto basi sehemu yao ni thumni ya mlicho kiacha, baada ya wasia mlio usia au kulipa deni. Na ikiwa mwanamume au mwanamke anaye rithiwa hana mtoto wala wazazi, lakini anaye ndugu mume au ndugu mke, basi kila mmoja katika hawa atapata sudusi. Na wakiwa zaidi kuliko hivyo basi watashirikiana katika thuluthi, baada ya wasia ulio usiwa au kulipa deni, pasio kuleta dhara. Huu ndio wasia ulio toka kwa Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi na Mpole. info

Fungu la mume ni nusu ya alicho acha mke ikiwa huyo mke hakuacha mtoto kutokana na mume huyo au mwenginewe. Akiwa huyo mke ana mtoto, basi mumewe atapata robo baada ya kutolewa wasia aliye uusia huyo mwanamke au kulipwa deni lake. Na fungu la mke au wake ni robo ya alicho acha mume ikiwa hakuacha mtoto kwa wake hao au wenginewe. Akiwa anaye mwana kutokana na hao au wake wenginewe basi mke huyu au wake hawa watapata thumni ya tirka baada ya wasia alio usia au deni. Na mwana wa mwana, yaani mjukuu, ni kama mwana katika haya yaliyo tangulia. Na akiwa maiti ni mwanamume au mwanamke, naye hana mwana wala mzazi, na kamwacha ndugu mume kwa mama, au ndugu wawili wa kike kwa mama, basi kila mmoja wao atapata sudusi, yaani sehemu moja katika sita. Na wakiwa wengi kuliko hivyo watashirikiana katika thuluthi, watagawana sawa sawa wanaume na wanawake kwa mujibu wa ushirika, baada ya kulipa madeni yaliyo kuwa juu yake, na kutimiza wasia ambao haudhuru urithi, nao ni wasia usio pindukia thuluthi iliyo baki baada ya kulipa madeni. Basi, enyi Waumini! Jilazimisheni kufuata aliyo kuusieni Mwenyezi Mungu; kwani Yeye hakika ni Mwenye kujua vyema nani miongoni mwenu anaye dhulumu na nani anaye fanya uadilifu, Yeye ni Mpole hafanyi haraka kutoa adhabu.

التفاسير:

external-link copy
13 : 4

تِلۡكَ حُدُودُ ٱللَّهِۚ وَمَن يُطِعِ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥ يُدۡخِلۡهُ جَنَّٰتٖ تَجۡرِي مِن تَحۡتِهَا ٱلۡأَنۡهَٰرُ خَٰلِدِينَ فِيهَاۚ وَذَٰلِكَ ٱلۡفَوۡزُ ٱلۡعَظِيمُ

Hiyo ni mipaka ya Mwenyezi Mungu. Na anaye mt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, Yeye atamtia katika Pepo zipitazo mito kati yake, wadumu humo. Na huko ndiko kufuzu kukubwa. info

Hizo ni hukumu zilizo tajwa kueleza khabari ya mirathi na mengine yaliyo tangulia ni Sharia za Mwenyezi Mungu aliye zipanga kwa ajili ya waja wake wazijue wala wasizikiuke. Na Mwenye kumt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume wake katika alivyo hukumu Yeye malipwa yake yatakuwa ni Pepo ipitayo mito kati yake, na atakaa humo daima dawamu. Na huko ndiko kushinda kukubwa. Mpango wa mirathi uliyo bainishwa na Qur'ani Tukufu ni mpango wa uadilifu na haki kuliko kanuni zote za mirathi nyenginezo duniani. Na haya wameyakiri wataalamu wa sharia wote wa Ulaya. Na huu ni mmoja katika ushahidi wa kuwa Qur'ani inatokana na Mwenyezi Mungu, kwani haya au yaliyo karibia haya hayakuwa yakijuulikana kwa Waajemi wala kwa Warumi wala katika sharia zozote za kabla ya Uislamu. Na sharia hii ya Kiislamu imefuata mipango hii ya uadilifu: Kwanza - Umefanywa urithi kwa mujibu apendavyo Mwenyezi Mungu, sivyo apendavyo mwenye mali, bila ya kupuuza kabisa mapenzi yake huyo. Amepewa huyo ruhusa ya kufanya wasia kwa thuluthi ya mali kwa ajili ya mambo mema, kama kutimiza kasoro katika waajibu wake wa dini, kama Zaka ambazo alikuwa hakuzitoa, au kuwajaalia kitu wahitaji alio khusiana nao kwa ujamaa au mapenzi nao hawastahiki urithi. Na amezuiliwa kufanya wasia ikiwa hayo yatapelekea maasi au yatachochea kuendelea maasia. Na thuluthi mbili zilizo baki baada ya wasia, au mali yote ikiwa hapana wasia, Mwenyezi Mungu Mtunga sharia, amejipa Yeye kuzigawa kwa haki. Pili - Katika kuchukua madaraka ya ugawaji tirka, Mwenyezi Mungu Aliye takasika, amempa aliye karibu zaidi kuliko mwenginewe, bila ya kuzingatia ukubwa au udogo. Kwa hivyo ndio ikawa watoto wana sehemu kubwa zaidi katika mirathi, kwani wao ndio kiendelezo cha yule maiti, na pia kuwa wao aghlabu ni wanyonge. Juu ya hivyo hawakukoseshwa, bali wameshirikiana nao, mama na bibi, baba na babu, ijapokuwa wanachukua akalli kuliko watoto. Tatu - Yaonekana kuwa mirathi ni kwa kadri ya haja. Kwa hivyo sehemu ya watoto ni kubwa kwa sababu haja yao ni kubwa zaidi, na wao ndio wanayakabili maisha, na kina baba na mama wanayapa mgongo maisha. Ama zingatio la haja ndilo lililo pelekea kuwa fungu la mwanamke liwe nusu ya fungu la mwanamume katika aghlabu ya hali za mirathi. Haya ni kwa kuwa mwanamume inambdi zaidi kukabili matumizi, kwa kuwa yeye anatakikana awalishe watoto na awatazame, amtumilie mwanamke. Maumbile ya kibinaadamu yamemfanya mwanamke ndiye asimamie kazi za nyumbani na kulea watoto, kuangalia raha zao, na mwanmume awe ni wa kuhangaika nje kiuchumi alete fedha za kutumia nyumba nzima. Kumpa kila mmoja kwa kadri ya haja ndio uadilifu. Kuweka sawa kwa wenye haja mbali mbali ni udhalimu. Nne - Sharia ya Kiislamu katika kugawa kwake tirka ya maiti inakusudia kugawa sio kurundika. Kwa hivyo haikufanya urithi wende kwa mtoto mkubwa peke yake, wala haikuwapa wanaume tu na kuwachilia mbali wanawake, wala watoto wakaachwa wazazi. Wala hawakukoseshwa wasio kuwa katika uti wa nasaba, kama ndugu, na maami, na banu-ami n.k. Urithi unaendelea mpaka kwa wanao karibia ukoo, lakini aliye karibu hufadhilika zaidi. Na shida kutokea kuwa mrithi ni mmoja tu. Tano - Mwanamke hakoseshwi kurithi, kama ilivyo kuwa ada ya Waarabu. Hivi ni kumhishimu mwanamke na kumpa haki yake. Na juu ya haya Uislamu hauzuii kurithi ujamaa wa mwanamke, bali hurithi jamaa walio kuwa upande wake, kama wanavyo rithi jamaa upande wa baba. Makaka na madada kwa upande wa mama wanachukua pale wanapo chukua ndugu wa baba na mama, bali katika hali nyengine wanachukua watoto wa kwa mama na kuchukua ndugu wanaume na wanawake. Na haya bila ya shaka ni kuutukuza umama, na kuutambua ukaribu wake. Haya hayakuwa yakijuulikana kabla yake, walakini hii ni Sharia ya Mwenyezi Mungu aliye Mjuzi na Mwenye hikima.

التفاسير:

external-link copy
14 : 4

وَمَن يَعۡصِ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥ وَيَتَعَدَّ حُدُودَهُۥ يُدۡخِلۡهُ نَارًا خَٰلِدٗا فِيهَا وَلَهُۥ عَذَابٞ مُّهِينٞ

Na anaye muasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na akaipindukia mipaka yake, (Mwenyezi Mungu) atamtia Motoni adumu humo, na atapata adhabu ya kudhalilisha. info

Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake na akaikiuka mipaka aliyo iweka Mwenyezi Mungu, na huku akihalalisha kukiuka huko basi mtu huyo atalipwa Moto, na humo atakaa milele, akiadhibiwa mwili wake juu ya kuadhibiwa roho yake.

التفاسير: