Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi zaidi kuliko nyinyi kuwajua maadui zenu wa kweli, na anatambua zaidi yaliyo ndani ya nafsi zao. Ulinzi wa Mwenyezi Mungu unakulindeni, na unakuangalieni, na unakutosheni. Basi msitafute ulinzi wa mwenginewe usio kuwa wake. Msaada na nusura yake inakutoshelezeni; basi msiwe kutaka msaada wa mwenginewe.
Miongoni mwa Mayahudi kipo kikundi kazi yao kugeuza geuza maana ya maneno. Wao husema kimoyomoyo kumwambia Mtume s.a.w.: Tumesikia hayo maneno, na hatuifati hiyo amri. Na pia husema: Sikia maneno yetu - hukusikia wito. Wakikusudia kwa hayo kumuapiza Mtume. Na husema: Sikia bila ya kusikilizwa. Tamko hilo wanalipindua maana. Muradi wao ni kumuapiza, na wanajidai kuwa muradi wao ni kumwombea dua. Na husema: "Raai'na", wakipindua ndimi zao wakijitia kuwa wanakusudia "Undhurna" yaani "Tuangalie". Wanaonyesha kuwa wanataka uangalizi wake, na kumbe wanakusudia neno la Kiyahudi lenye maana ya "Mpumbavu" ili kuibeza Dini ya Kiislamu. Na lau kuwa wangeli nyooka sawa wakasema: "Tumesikia na tumet'ii" badala ya hiyo kauli yao ya "Tumesikia na tumeasi", na wakasema: "Sikia" na wasiseme "Bila ya kusikilizwa", na wakasema :"Undhurna" yaani "Tuangalie", badala ya "Raa'ina", ingeli kuwa bora kwao kuliko hayo wayasemayo, na ingeli kuwa ndiyo njia ya uadilifu zaidi. Lakini Mwenyezi Mungu amewatoa katika rehema yake kwa ule upinzani wao. Kwa hivyo huwaoni miongoni mwao wanao mwitikia mwenye kuwaitia Imani ila wachache tu.
Enyi mlio pewa Kitabu alicho teremsha Mwenyezi Mungu! Iaminini Qur'ani tuliyo mteremshia Muhammad, inayo sadikisha mliyo nayo, kabla hatujawateremshia adhabu ya kufutwa nyuso zenu zikawa kama visogo, hazina pua, wala macho, wala nyusi. Au tukakutoeni katika rehema yetu kama tulivyo watoa wale walio ikhalifu amri yetu wakatenda waliyo katazwa ya kuvua samaki siku ya mapumziko,(Sabt au Sabato) siku ya Jumaamosi. Na hukumu ya Mwenyezi Mungu ni yenye kutimizwa tu, wala hapana cha kuipinga.
Hakika Mwenyezi Mungu hafuti dhambi za ushirikina, kumfanya Yeye ana mshirika yeyote. Na husamehe dhambi zilio chini ya huo ushirikina kwa amtakaye miongoni mwa waja wake. Na mwenye kumshirikisha Mwenyezi Mungu basi amemzulia Mwenyezi Mungu na ametenda dhambi kubwa mno isiyo stahiki kusamehewa.
Hustaajabii hali ya hao makafiri wanao zua kwa vitendo vyao? Vitendo vyao viovu wao wanaviona kuwa ni vizuri. Wanajisifu kuwa kwa vitendo hivyo wao wametakasika. Na ni Mwenyezi Mungu tu peke yake ndiye anaye jua jema na baya. Yeye ndiye wa kumtakasa amtakaye, na wala hamdhulumu mtu yeyote kadiri yake hata chembe.
Vipi watu hawa wanavyo mzulia Mwenyezi Mungu uwongo kwa haya na mengineyo mfano wa haya! Yatosha uwovu ulio wazi kwa huu uwongo wao kuyakashifu maovu yao.
Hebu huwastaajabii hawa walio pewa sehemu ya ujuzi wa Kitabu wanavyo ridhia ibada ya masanamu na Shetani, na wanavyo sema kuwa hao waabuduo masanamu ni afadhali wameongoka kwenye Njia kuliko Waislamu wenye kuamini?