Katika Qur'ani ipo Ishara inayo thibitisha ukweli wako. Basi wao wakisema, kuwa hii umeitunga wewe na umemzulia Mwenyezi Mungu, wewe waambie: Ikiwa Qur'ani hii imetokana na mwanaadamu, basi yamkinika mwanaadamu mwengine kuleta mfano wake. Na nyinyi ni mafasihi kuliko wote. Basi leteni Sura kumi kama hii mbali mbali, na mtakeni msaada yeyote mnaye weza kumtaka, katika watu na majini, kama hakika mnasema kweli katika hayo madai yenu kuwa haya ni maneno ya binaadamu. Qur'ani si muujiza tu katika maandishi yake, bali ndani yake mna hadithi za kweli, na ilimu mbali mbali za sayansi za uumbaji zilizo ashiriwa, na hazikuwa zikijuulikana wakati wa kuteremka kwake, na pia katika hukumu ziliomo ndani yake.
Mkishindwa, na wakashindwa mlio wataka msaada, kuleta mfano wake hii wa kuzua, basi jueni kuwa Qur'ani haikuteremshwa ila kwa kuambatana na ujuzi wake Mwenyezi Mungu. Ilimu yake haijui mtu ila Yeye. Na jueni kuwa hapana mungu ila Allah, Mwenyezi Mungu tu. Hapana anaye tenda kazi yake. Basi kuweni Waislamu baada ya kwisha thibiti hoja hizi juu yenu, kama nyinyi mnataka Haki.
Wenye kutaka uhai wa duniani, na kustarehea ladha zake na pumbao lake, tutawapa matunda ya vitendo vyao bila ya nuksani.
Hao ambao hima yao ni kushughulikia dunia tu, Akhera hawana lao jambo ila adhabu ya Motoni, na kuharibikiwa na yote waliyo yafanya duniani, kwa sababu hawakuwa na fungu lolote katika Akhera. Na hayo wayatendayo pia yatakuwa yameharibika vile vile, kwani kitendo kisicho leta mafanikio ya daima ni kama kwamba hakikupata kuweko.
Je, anaye kuwa anakwenda katika maisha yake kwa uangalifu na uwongofu kutokana na Mola wake Mlezi, na anaitaka Haki kwa kuifanyia ikhlasi, pamoja naye anaye shahidi anaye mshuhudia kuwa kweli katoka kwa Mwenyezi Mungu, naye shahidi huyo ni Qur'ani, na shahidi wa kabla yake ni Kitabu cha Musa alicho kiteremsha Mwenyezi Mungu kiwe ni uwongozi wa kufuatwa kwa aliyo yaleta, na ni rehema kwa wenye kukifuata, je, huyo ni sawa sawa na anaye kwenda katika maisha yake katika giza na upofu, hashughulikii ila starehe za duniani tu na pumbao lake? Hao walio tajwa mwanzo ndio wale ambao Mwenyezi Mungu ameyatia nuru macho yao. Wanamuamini Nabii huyu, na Kitabu alicho teremshiwa. Na wenye kumkataa wakakusanyika na kujiunga dhidi yake, basi Moto ndio pahali pa miadi yao Siku ya Kiyama. Ewe Nabii! Usiwe na shaka na hii Qur'ani. Hii ni kweli itokayo kwa Mola wako Mlezi. Haingii upotovu. Lakini watu wengi wanapotezwa na matamanio, basi hawaamini kama iwapasavyo. Mwenyezi Mungu amemuamrisha Nabii s.a.w. asitie shaka, si kwa kuwa yawezekana kuwa yeye awe na shaka, lakini ni kuashiria kuwa walio kuwa duni yake Nabii wajilinde wasiache shaka ikaingia nyoyoni mwao.
Hapana walio zidi kujidhulumu nafsi zao na wakajitenga mbali na Haki kuliko wale wanao tunga uwongo, na kisha wakamnasibishia Mwenyezi Mungu. Hakika watu hawa Siku ya Kiyama watadhihirishwa mbele ya Mola wao Mlezi awahisabie kwa yale maovu waliyo yatenda. Mashahidi miongoni mwa Malaika, na Manabii, na wengineo, watasema: Hawa ndio walio tenda makosa maovu kabisa na dhulma kwa mintarafu ya Muumba wao! Hapana shaka laana ya Mwenyezi Mungu itawapata hao kwa kuwa ni wenye kudhulumu.
Hawa ndio wanawageuza watu wasiifuate Dini ya Mwenyezi Mungu, na wanawazuia. Nayo hiyo ndiyo Njia yake Iliyo Nyooka. Na wanataka Njia hii iwafikiane na matamanio yao na pumbao lao, kwa hivyo yende upogo. Hao wanaikanya Akhera, na yaliyomo ndani ya kulipwa thawabu Muumini na kuadhibiwa kafiri.