Enyi watu! Tahadharini na adhabu ya Mola wenu Mlezi, na wekeni katika nyoyo zenu makumbusho ya Siku ya Kiyama. Kwani mtingishiko utao tokea hapo ni mkubwa, wenye kuhangaisha na kutikisa viumbe.
Siku mtapo kiona Kiyama mtaona kitisho chake kinafikilia ukubwa wake hata kama yupo mwanamke anaye nyonyesha na ziwa lake limo katika mdomo wa mwanawe, basi hapana shaka atamsahau na amwachilie mbali. Na kama yupo mwanamke ana mimba basi ataiharibu mimba kabla ya kufika wakati wake wa kuzaa kwa ajili ya fazaa na kitisho. Na ewe mwenye kuangalia! Ukiona hali ya watu Siku hiyo namna wanavyo onekana hawanazo, na wanapo kwenda wanayumba, utadhani wamelewa, na ilhali hawakulewa. Lakini kitisho walicho kishuhudia, na khofu ya adhabu kuu ya Mwenyezi Mungu ndiyo iliyo waondoshea utulivu wao.
Na juu ya onyo hili kali na la kweli bado wapo baadhi ya watu inadi yao au kufuata kwao kijinga huwapelekea katika mambo ya kubishana juu ya Mwenyezi Mungu na sifa zake, wakamsingizia kuwa ati ana washirika, au wakaukataa uweza wake wa kufufua na kuwalipa watu kwa vitendo vyao. Na kwa huo ubishi wao na kukataa kwao hawategemei ilimu sahihi, au hoja ya kweli; lakini wao hufuata tu nyayo za kila shetani aliye muasi Mola wake Mlezi, aliye baidika na uwongofu.
Mwenyezi Mungu amehukumu kuwa anaye mfuata Shetani na akamfanya kuwa ni rafiki yake na mlinzi wake, na mwongozi wake, basi humpotoa na njia ya Haki, na akamuelekeza kwenye upotovu unao pelekea kwenye Moto unao waka na kuripuka.
Enyi watu! Ikiwa nyinyi mna shaka ya kukufufueni baada ya kufa, basi katika kuumbwa kwenu ipo dalili ya kuweza kwetu kufufua. Tulikuumbeni asili yenu kutokana na udongo, kisha tukaufanya tone ya manii, kisha baada ya muda tukaigeuza ikawa kipande cha damu iliyo gandana. Kisha tukaifanya kipande cha nyama yenye sura ya kibinaadamu, au isiyo kuwa na sura, ili tukubainishieni uweza wetu wa kuanza uumbaji na kuendeleza kukuza kwa viwango na madaraja, na kugeuza kutoka hali hii na kuingia nyengine. Na katika viliomo katika matumbo ya mzazi vipo tunavyo viharibu tuvitakavyo na tunaviweka imara na madhubuti tuvitakavyo, mpaka utimie muda wa kuzaliwa. Kisha tunakutoeni kwenye matumbo ya mama zenu muwe watoto wachanga. Kisha tunakuleeni mpaka mkamilike akili na nguvu. Na baada ya hayo wapo katika nyinyi ambao Mwenyezi Mungu huwafisha, na wapo ambao umri wao hurefushwa mpaka wakafikia ukongwe wa kupiswa, ujuzi wao na kufahamu kwao mambo kukasita. Na aliye kuumbeni kwa sura hii tangu mwanzo hashindwi kukurudisheni tena. Na jambo jengine la kukuonyesha kudra ya Mwenezi Mungu kufufua ni kuwa wewe unaiona ardhi kavu yabisi; tukiiteremshia maji uhai unaitambalia, na hiyo ardhi hugutuka, na huzidi na hututumka kwa maji na hewa iliyo ingia ndani yake, na hapo tena hutokeza namna mbali mbali za mimea inayo furahisha kuiona, na uzuri wake ukazagaa, na mwenye kuiona roho yake ikakunjuka. (Maurice Bucaille, mtaalamu wa Kifaransa maarufu aliye silimu, amelifasiri neno A'laqa kwa maana ya "kitu kilicho tundikwa". Na hivyo ndivyo inavyo thibitisha Sayansi ya hivi sasa, kuwa mbegu ya uzazi ikisha pandikizwa huja ikaning'inia kama iliyo tundikwa kwenye tumbo la uzazi. Tazama pia 23.14, 40.67, 75.37-38 na kadhaalika Sura ya 5 ya Annisaa Aya 129, inayo eleza kuwa msimwache mke "kama aliye tundikwa")