Hivyo basi haiwapitikii watu hawa na wale kuwa Mwenyezi Mungu hana haja ya kupata hoja kama hizo? Kwani Yeye anajua wanacho kificha na wanacho kidhihirisha.
Na miongoni mwa Mayahudi kipo kikundi cha wajinga wasio jua kusoma, wasio jua chochote kutokana na Taurati ila uwongo unao wafikiana na matamanio yao, wanao wapachikia pachikia makohani wao, na wakaona katika mawazo yao kuwa hayo ni kweli iliyotoka Kitabuni.
Basi hao makohani wataangamia na watapata adhabu kwa vile wanavyo andika vitabu kwa mikono yao, kisha wakawaambia wajinga wasiojua kusoma kuwa: Hii ni Taurati iliyo toka kwa Mwenyezi Mungu. Kusudi lao ni kuwa wapate kwa hayo pato la upuuzi la kidunia, wanunue upuuzi huu kwa kuuza Haki na Kweli. Basi ole wao kwa wanayo mzulia Mwenyezi Mungu, na ole wao kwa yale matunda wanayo yachuma kwa uzushi wao!
Na katika khitilafu zao ni haya wanayo yapata kwa makohani ya kuwa Moto hautawagusa Mayahudi hata wakifanya maasia namna gani ila kwa muda wa siku chache tu. Basi waambie ewe Muhammad!: Nyinyi mmeagana na Mwenyezi Mungu kwa hayo, hata mkawa mmetumaini kuwa Mwenyezi Mungu havunji ahadi yake, au mnamzulia uwongo tu?
Ukweli wa mambo ni kuwa nyinyi mnamzulia Mwenyezi Mungu uwongo. Kwani hukumu ya Mwenyezi Mungu inapitishwa kwa viumbe vyake vyote sawa sawa, hapana farka baina ya Yuhudi na asiye kuwa Yahudi. Wenye kutenda maovu, na maovu yakawazunguka hao waovu mpaka njia za kuokoka zote zikazibwa, basi hao ndio watu wa Motoni na huko watudumu milele.
Na wale walio amini na wakatenda mema hao ndio watu wa Peponi, kwa sababu wao wameamini na wakatimiza iliyo wajibisha Imani yao, nayo ni vitendo vyema, basi wao watakaa Peponi daima milele.
Mbali na haya yote, nyinyi jamaa wa Kiyahudi, mnaendelea kuyashughulikia madhambi na kuvunja ahadi, na kupindukia mipaka aliyo kuwekeeni Mwenyezi Mungu. Kumbukeni tulipo chukua ahadi kwenu katika Taurat kuwa hamtamuabudu ila Mwenyezi Mungu, na mwatendee wema wazazi na jamaa na mayatima na masikini, na mnapo zungumza na watu mtumie maneno mazuri ya kuleta masikilizano baina yenu nao wala sio ya kukutenganisheni, na mtimize yaliyo kuwa waajibu juu yenu, nayo ni Swala, na Zaka. Na kumbukeni ulikuwaje mwendo wenu katika ahadi hiyo? Vipi mlivyo ivunja na mkajipuuza nao, isipo kuwa wachache tu ndio walio ifuata Haki?