Na kumbukeni tulipo chukua ahadi kwenu katika Taurat kuwa hamtakuwa mkimwaga damu zenu, wala hamtafukuzana katika majumba yenu. Na ahadi hiyo mnakubali kuwa ipo katika Kitabu chenu na mnashuhudia kuwa ni kweli.
Nanyi wenyewe kwa wenyewe mnauwana, na mnatoana majumbani, nyinyi kwa nyinyi: hawa wanawauwa hawa na hawa wanawauwa hawa; hawa wanawafukuza hawa majumbani mwao na hawa wanawafukuza hawa. Na huku mkisaidiana katika vitendo vya dhambi na uadui. Baada ya hayo wakitokea baadhi yenu wakatekwa na hao mnao shirikiana nao mnajishughulisha kwenda kuwakomboa hao mateka. Mkiulizwa nini kilicho kupelekeeni kuwakomboa, mnajibu kuwa vitabu vyenu vinakuamrisheni kukomboa mateka wa Kiyahudi. Jee, vitabu hivyo havikukuamrisheni msimwage damu ya ndugu zenu? Havikukuamrisheni msiwatoe watu majumbani mwao? Hivyo nyinyi mnat'ii sehemu ya yaliyo kujieni katika Kitabu na mnayakataa mengineyo? Basi jaza ya mwenye kutenda hayo katika nyinyi si lolote ila kupata hizaya katika maisha ya duniani, na Siku ya Kiyama. Mwenyezi Mungu, anaye vijua vyema vitendo vyao na siri zao, atawapeleka kwenye adhabu iliyo kali kabisa. Kabla ya Uislamu zilikuwapo katika mji wa Madina kabila mbili za Kiarabu ambazo zilikuwa na uadui baina yao, nazo ni Aus na Khazraj. Na pia zilikuwako kabila za Kiyahudi nazo ni Banu Quraidha na Banu Nnadhir. Banu Quraidha walifungamana na Aus, na Banu Nnadhir walifungamana na Khazraj. Ilikuwa kabila mbili za Kiarabu zikipigana, zile kabila za Kiyahudi nazo huingia vitani, kila kabila upande wa rafiki zake, na zikiuwana na wenzao wa dini moja nao, na wakifukuzana makwao. Lakini kila moja katika kabila mbili hizo za Kiyahudi zikishughulika baadaye kuwakomboa mateka walio tekwa na rafiki zao wa Kiarabu. Wakiulizwa kwa nini mnawakomboa na hao walikuwa wakipigana nanyi upande wa maadui zenu? Wao wakisema: Mwenyezi Mungu ametuamrisha katika Taurati tuwakomboe mateka wa Kiyahudi. Na wanajifanya hawajui kama Mwenyezi Mungu amewaamrisha vile vile wasiuwane wala wasitoane majumbani mwao. Kwa hivyo ndio wanaamini sehemu ya Kitabu na wanaikataa nyengine.
Na hayo ni kwa kuwa wamekhiari mapato ya hii dunia ipitayo kuliko neema za Akhera zitakazo dumu. Katika haya wamekuwa kama mtu aliye uza Akhera yake kwa ajili ya kununua dunia. Basi hawatapunguziwa adhabu ya Jahannam, wala hawatapata wa kuwaokoa nayo.
Enyi Mayahudi, kumbukeni vile vile, ule msimamo wenu wa upotovu na wenye dhambi kwa mnasaba wa Musa na Mitume mingine tulio watuma. Kwani tulimtuma kwenu Musa na tukampa Taurati, na kumfwatia yeye tuliwaleta Mitume kadhaa wa kadhaa wengineo. Miongoni mwao ni: Isa bin Maryamu ambaye tulimpa miujiza na tukamuunga mkono kwa Roho Mtakatifu, naye ni Jibril Mjumbe muaminifu wa Ufunuo. Nanyi kila akikujilieni Mtume asiye wafikiana na matamanio yenu mnatakabari na hamtaki kumfwata. Mitume wengine mliwakataa na kuwaambia waongo, na wengine mliwauwa khasa.
Hali kadhaalika msimamo wenu kwa Mtume wetu Muhammad, Nabii wa mwisho. Mlimwambia alipo kuiteni msilimu: Nyoyo zetu zimefunikwa kwa vifuniko visivyo achilia kupenya huo wito wako. Basi sisi hatuelewi kitu chochote unacho sema! Wala nyoyo zao hazikufunikwa kama wanavyo dai, lakini wamepanda kiburi tu, na wakakhiari upotovu kuliko uwongofu. Basi Mwenyezi Mungu amewalaani kwa ukafiri wao, na amedhoofisha yakini yao na imani yao.