Enyi Mayahudi, kumbukeni vile vile, ule msimamo wenu wa upotovu na wenye dhambi kwa mnasaba wa Musa na Mitume mingine tulio watuma. Kwani tulimtuma kwenu Musa na tukampa Taurati, na kumfwatia yeye tuliwaleta Mitume kadhaa wa kadhaa wengineo. Miongoni mwao ni: Isa bin Maryamu ambaye tulimpa miujiza na tukamuunga mkono kwa Roho Mtakatifu, naye ni Jibril Mjumbe muaminifu wa Ufunuo. Nanyi kila akikujilieni Mtume asiye wafikiana na matamanio yenu mnatakabari na hamtaki kumfwata. Mitume wengine mliwakataa na kuwaambia waongo, na wengine mliwauwa khasa.