Na vijana vyenu wakifikilia umri wa kubalighi inawapasa watake ruhusa ya kuingia kila nyumba, na kila wakati, kama ilivyo wapasa wenzao wa kabla yao. Na kwa mfano wa uwazi kama huu Mwenyezi Mungu anakuwekeeni wazi Aya zake alizo ziteremsha. Na Mwenyezi Mungu Subhanahu ni Mkunjufu wa ujuzi, Mkubwa wa hikima. Anajua linalo wasilihi waja wake, na anawaatungia Sharia zinazo wanasibu, na kwa kadri ya haja yao.
Na wanawake wakongwe ambao hawatumai kuolewa, hawalaumiwi wakipunguza baadhi ya nguo zao, kwa sharti wasiwe wanajishauwa kwa kuonyesha uzuri wa mwili wao ambao Mwenyezi Mungu ameamrisha usitiriwe. Lakini kujihishimu kwa kujisitiri kwa ukamilifu ni bora kwao kuliko kujifunua. Na Mwenyezi Mungu anawasikia wayasemayo, na anayajua makusudio yao, na atawalipa kwa hayo.
Wenye udhuru kama vile vipofu, viguru, wagonjwa hawana lawama, bali hata nyinyi wazima hamna lawama kula katika nyumba za watoto wenu, kwani hizo ni nyumba zenu. Wala kula katika nyumba za baba zenu, na mama zenu, na ndugu zenu wanaume na ndugu zenu wanawake, au nyumba za ami zenu, au mashangazi zenu, au wajomba zenu, au mama wadogo, dada wa mama zenu, au nyumba ambazo mmewakilishwa kuzitazama, au nyumba za rafiki zenu mnao changanyika nao, ikiwa hamna yaliyo harimishwa humo. Na hayo ikijuulikana kuwa mwenye nyumba ameruhusu yeye au mkewe. Wala hapana ubaya kula humo pamoja au mbali mbali. Na muingiapo katika nyumba toeni salamu kwa waliomo ambao hao ni baadhi yenu kwa umoja wa Dini na ujamaa. Kwani hao ni kama nyinyi. Na maamkio haya ni maamkio yaliyo wekewa Sharia, yenye baraka na thawabu, na pia ndani yake nyoyo hupoa. Na kwa mfano kama huu Mwenyezi Mungu anazifafanua Aya kwa ajili yenu mpate kuelewa waadhi na hukumu ziliomo ndani yake, na mpate kuzifahamu na mzitende.