Dunia na yaliomo duniani ya kuuza na kununua hayawashughulishi wakaacha kumdhukuru Mwenyezi Mungu na kumzingatia. Wao wanashika Swala, na wanatoa Zaka, na huku wakiikhofu Siku ya Kiyama ambapo nyoyo zitakuwa hazina utulivu kwa sababu ya wasiwasi na hamu, na kungojea matokeo, na macho yatadahadari kwa mhangaiko na kushtuka kwa vituko vigeni wanavyo viona, na wingi wa vitisho.
Na malipo ya vitendo vyao ni kulipwa sawa sawa kwa ubora wa malipo kwa vitendo vyao vyema, na watapata fadhila kwa kupewa zaidi kuliko wanavyo stahiki. Kwani Yeye Subhanahu ni Mkunjufu wa fadhila, humpa amtakaye katika waja wake wema kipao kikubwa, asichoweza mtu kukihisabu wala wenye kuhisabu hawawezi kukisia.
Na hao walio pinga na wakakanya wanadhani wenyewe kuwa wamefanya vizuri, na kwamba vitendo vyao vizuri vitawaletea faida Siku ya Kiyama. Lakini hao wamekosea katika dhana yao hiyo. Kwani mfano wa vitendo vyao katika upotovu wake na kukosa maana ni kama mmetuko unao tokea unapo angukia mwako wa jua wakati wa adhuhuri juu ya ardhi tambarare jangwani. Mwenye kiu hudhania kuwa ni maji. Hata akiyafikia asikute chochote chenye manufaa kama alivyo dhania. Hali kadhaalika vitendo vya makafiri siku ya malipo vitakuwa vumbi lilio tawanyika. Na kafiri ataikuta adhabu ya Mwenyezi Mungu inamngojea kwa utimilivu wake bila ya nuksani. Hakika hisabu ya Mwenyezi Mungu hapana shaka inakuja. Na Yeye, Aliye takasika, ni Mwepesi katika kuhisabu kwake, hachelewi wala hakosei.
Na huu mfano mwengine wa vitendo vya makafiri. Mfano wake ni mfano wa giza la bahari kubwa iliyo tanda yenye kina kirefu. Mawimbi yake yanapigana na kusukumana wenyewe kwa wenyewe. Nayo yamefunikwa na mawingu mazito meusi hayapitishi mwangaza. Katika giza hili lililo rundikana msafiri wa baharini hawezi kuuona mkono wake hata akiukurubisha machoni. Basi anabaki ameduwaa amebabaika hajijui. Na vipi ataona kitu atokane na butaa hili bila ya kupata Nuru ya kumwongoa katika mwendo wake, na kumwokoa na kugongana na kuhiliki. Na basi kama hali hiyo hiyo makafiri hawapati faida katika vitendo vyao, wala hawatoki katika upofu wao na upotovu wao, wala hawajiokoi nafsi zao, ila kwa Nuru ya Imani. Kwani hana Nuru ya kumwongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka. Basi atakuwa katika walio teketea. "Na walio kufuru vitendo vyao ni kama sarabi (mazigazi) uwandani. Mwenye kiu huyadhania ni maji. Hata akiyaendea hapati chochote. Na atamkuta Mwenyezi Mungu hapo naye amlipe hisabu yake sawa sawa. Na Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu." Sarabi si chochote ila mandhari ya mwangaza yanayo sabibishwa na marejeo (reflection) ya miale inayo toka kwenye vitu vyenye kutoa mwanga. Na hiyo hurejeshwa tena kutokana na ardhi pana tupu, yaani uwanda, na kupanda kidogo kidogo mkabala na uso wa ardhi, na joto linapo panda wakati wa mchana, basi miale hiyo inayo rejea ikifika kwa jicho la mwenye kuangalia huona vile vitu vimegeuka juu chini kama kwamba kwenye kiyoo kikubwa kilicho tanda. Na kadhaalika mbingu safi ya rangi ya kibuluu huonekana kama kwamba ni ziwa la maji juu ya uso wa ardhi. Na vile vitu vingine kama miti miti na mitende iliyo onekana juu chini inazidi kuonyesha kama kwamba ni vivuli kwenye maji. Na hii Sarabi huzidi kudhihiri kwa uwazi kabisa inapo kuwa khitilafu ni kubwa baina ya joto la uso wa ardhi na angani katika hewa. Na hayo huonekana zaidi majangwani na nyandani na kwenye barabara za jangwani za lami zilio nyooka. Kwa maelezo hayo inaonekana kuwa Sarabi ni kiini macho tu. Maoni ya wataalamu juu ya Aya 40: " Au ni kama giza katika bahari kuu, iliyo funikwa na mawimbi juu ya mawimbi, na juu yake yapo mawingu. Giza juu ya giza. Akiutoa mtu mkono wake anakaribia asiuone. Na ambaye Mwenyezi Mungu hakumjaalia kuwa na nuru hawi na nuru." Aya hii tukufu imekusanya yaliyo muhimu kabisa katika midharuba ya baharini. Ni maarufu kuwa midharuba ya bahari kuu huwa na mawimbi yanayo khitalifiana urefu wao na ukubwa wao au mnyanyuko wao, hata inaonekana kama kwamba hayo mawimbi yanapandana moja juu ya mwenzie, na kwa hivyo yakaziba mwangaza wa jua kwa vile hiyo midharuba inasabibisha kurundika kwa mawingu mazito ambayo nayo huuziba mwangaza wa jua, na kwa hivyo husabibisha giza mtu asiweze kuona kitu juu ya kuwa macho yake mazima. Na ilivyo kuwa Mtume s.a.w. kazaliwa na kakulia jangwani, kuja maelezo kama haya ya undani ya ki-ilimu kwa ulimi wake kuwa ni ufunuo ulio tokana na Mwenyezi Mungu, ni ushahidi kuwa Qur'ani inatoka kwa Mwenyezi Mungu, na kuwa ni muujiza wa Mtume huyu mtukufu.
Ewe Nabii! Hujui kwa yakini kwamba kwa Mwenyezi Mungu hunyenyekea kila kiliomo mbinguni na duniani? Na wanamnyenyekea ndege vile vile, nao wamekunjua mbawa zao? Basi viumbe vyote hivi vinanyenyekea amri ya Mwenyezi Mungu na mipango yake. Vinamtakasa na washirika na kila lisio na laiki naye. Na kila kimojawapo kinajua kwa kujaaliwa na Mwenyezi Mungu yaliyo kiwajibikia katika unyenyekevu na kutakasa na kutimiza wadhifa wa maisha. Na Mwenyezi Mungu nyuma yao anajua kwa utimilivu wa kujua Swala ya kila mwenye kusali, na kusabihi kwa mwenye kusabihi, na yote wayafanyayo waja. Basi huwaje makafiri wakawa hawaamini?
Na Mwenyezi Mungu peke yake ndiye Mwenye kumiliki mbingu na ardhi na viliomo ndani yao, na ndiye Mwenye madaraka juu yao, na wote watarejea kwake Siku ya Kiyama kwa ajili ya hisabu na malipo.
Ewe Nabii! Huoni kwamba Mwenyezi Mungu huyavuta mawingu, kisha huyakusanya na kuyarindika moja juu ya moja. Utaona mvua inatoka kwenye mawingu. Na Mwenyezi Mungu huteremsha kutokana na mawingu yaliyo rindikana yanayo shabihi milima kwa ukubwa wake, vipande vya barafu kama changarawe, vikawaangukia watu vikawaletea manufaa au madhara, kufuatana na kanuni zake na matakwa yake, wala asiwateremshie wenginewe kwa mujibu apendavyo Yeye Subhanahu, Mtendaji, Mwenye kukhitari. Mwangaza wa umeme unao tokea kwa kugongana mawingu hukaribia kutia upofu kwa ukali wake. Na mambo kama haya ya kuonekana ni dalili za kuonyesha uwezo wa Mwenyezi Mungu ambao unao wajibisha kuleta Imani ya kumuamini Yeye. Hajui kushabihiana baina ya mawingu na milima ila mwenye kupanda ndege (eropleni) inayo ruka juu ya mawingu, akayaona kutoka huko juu kama ni milima na vilima. Ilivyo kuwa ndege hizo hazijawa bado zama za Mtume s.a.w. basi hii inakuwa ni dalili kuwa maneno haya yanatokana na Mwenyezi Mungu anaye jua ya juu na chini. "Je! Huoni ya kwamba Mwenyezi Mungu huyasukuma mawingu, kisha huyaambatisha, kisha huyafanya mirundi? Basi utaona mvua ikitoka kati yake. Na huteremsha kutoka juu kwenye milima ya mawingu mvua ya mawe, akamsibu nayo amtakaye na akamuepusha nayo amtakaye. Hukurubia mmetuko wa umeme wake kupofua macho." Aya hii tukufu imeutangulia msafara wa sayansi. Kwani hii yaeleza daraja za kuundika mawingu yanayo rindikana, na sifa zake, na yaliyo juulikana hivi karibuni ki-sayansi ya kwamba mawingu ya mvua huanzia kwa sura ya moja moja kisha yakajumuika yakawa kikundi, ndiyo hayo mawingu yaliyo rindikana, yaani mawingu yanayo endelea kukua kwa kuelekea utosini. Hayo hukua kimo chake hata kufikia urefu wa kilomita 15 au 20, na hapo huonekana kama ni milima mikubwa iliyo nyanyuka. Na yajuulikanayo ki-sayansi ni kuwa mawingu yaliyo rindika yanapitia daraja tatu, nazo: Daraja ya kukusanyika na kukua. Daraja ya kunyesha. Na mwisho daraja ya kumalizikia. Kama ilivyo kuwa mawingu hayo - nayo ni peke yao - yenye mvua ya mawe na inabeba nguvu za umeme (electricity, Kahrabaa) , huweza kuwa yakashika mfululizo wa umeme na radi, hata huweza ikawa ni miripuko karibu 40 kwa dakika moja, hata mtu anaye tazama akawa hawezi tena kuona kwa ukali wa mwanga wake. Na haya ndiyo khasa yanayo wapata marubani wa meli na ndege wakati wa midharuba ya radi.