Hakika hao walio zua uwongo ulio potoka na kila uwongofu kumzulia Aisha, mke wa Nabii s.a.w. walipo mtangazia uzushi, ni kikundi wanao ishi pamoja nanyi. Msidhani kituko hichi ni shari kwenu, bali ndiyo kheri yenu; kwa sababu kimewapambanua baina ya wanaafiki na Waumini wa kweli. Na ukadhihiri ukarimu wa walio wema na wenye kuingiwa na uchungu. Na kila mtu katika hawa walio tuhumu watapata malipo yao kwa mujibu wa kadri alivyo shiriki katika uzushi huu. Na mkuu wa kikundi hichi ndiye ataye pata adhabu kubwa kwa ukubwa wa makosa yake.
Ilikuwa inavyo takikana kwa Imani ni kuwa wakati wa kusikia huu uzushi, ni Waumini wanaume na wanawake wajidhanie nafsi zao kheri ya usafi na unadhifu, na waseme kwa kupinga: Huu ni uwongo ulio wazi umezuliwa, kwa kuwa haya yamemkhusu bora ya Mitume na bora ya wanawake walio wa kweli.
Je! Hao wazushi walileta mashahidi wane wa kushuhudia hayo waliyo yasema? Hawakufanya hayo...Na ikiwa hawakufanya basi hao kwa hukumu ya Mwenyezi Mungu ni waongo.
Na lau kuwa Mwenyezi Mungu hakukufanyieni fadhila kwa kubainisha hukumu, na hakukurehemuni duniani kwa kuacha kuleta adhabu kwa haraka, na Akhera kwa kukusameheni, angeli kuteremshieni adhabu kubwa kwa sababu ya kujiingiza kwenu katika uzushi huu.
Mmezichukua khabari hizo kwa ndimi zenu na mkazieneza kati yenu. Wala nyinyi hamkujua kuwa hizo ni khabari za kweli, na mkaona jambo hili ni dogo si la kuadhibiwa na Mwenyezi Mungu, au sana adhabu yake ni ndogo; na ilhali ni jambo kubwa kweli la kuadhibiwa adhabu kali na Mwenyezi Mungu.
Yanayo faa ni kuwa baada ya kusikia maneno haya ya uwongo ni kuambizana msiyazungumze, kwa sababu si laiki yenu, na mustaajabie kuzuliwa uwongo muovu wa namna hii wa khatari.
Na hakika Mwenyezi Mungu anakukatazeni msirudie tena kufanya maasi namna hii kabisa, ikiwa nyinyi ni Waumini wa kweli. Kwani sifa za Imani zinapingana na mwendo huu.
Na Mwenyezi Mungu anakuteremshieni Aya zenye kuonyesha hukumu kwa uwazi dhaahiri. Na Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu wa Ujuzi, hapana asicho kijua katika vitendo vyenu. Naye ni Mwenye hikima kwa kila anacho kitungia sharia na kukiumba. Kwani kila sharia zake na uumbaji wake ni kwa mujibu wa hikima.
Hakika hao wanao penda kutangaza machafu, wakayatangaza baina ya Waumini watapata adhabu yenye kutia uchungu duniani kwa mateso yaliyo kwisha pasishwa, na Akhera watatiwa Motoni ikiwa hawato tubu. Na Mwenyezi Mungu anazijua vyema hali zenu zote, za dhaahiri na zilizo fichikana. Na nyinyi hamjui anayo yajua Yeye.
Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake kwenu, na kuwa Yeye ni Mwingi wa upole, Mkunjufu wa rehema, asingeli kubainishieni hukumu, na angeli kuleteeni mateso kwa haraka hapa duniani kwa maasi yenu.