Watu wa Mūsā walisema kumwambia, «Hatutaungia mji huo kabisa, iwapo hao majabari wamo humo. Hivyo basi, nenda wewe na Mola wako mkapigane. Ama sisi, tunakaa hapa- hapa na hatutapigana na wao.» Hii inaonesha kushikilia kwao kuenda kinyume na Mūsā, amani imshukie.
Mwenyezi Mungu Alisema kumwambia Nabii Wake Mūsā, amani imshukie, «Hakika hiyo ardhi takatifu ni haramu kwa hawa Mayahudi kuiingia kwa muda wa miaka arubaini, watakuwa wakitanga katika ardhi wakiwa kwenye hali ya mshangao. Basi usiwasikitikie, ewe Mūsā, watu waliotoka kwenye utiifu wangu.»
Wasimulie, ewe Mtume, Wana wa Isrāīl habari ya wana wawili wa Ādam, Qābīl na Hābīl, nayo ni habari ya kweli, alipotoa kila mmoja wao sadaka, nayo ni ile inayotolewa ili kujisogeza karibu kwa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka. Hapo Mwenyezi Mungu Aliikubali sadaka ya Hābīl kwa kuwa alikuwa mcha-Mungu, na Hakuikubali sadaka ya Qābīl, kwa kuwa hakuwa mcha-Mungu. Qābīl alimhusudu ndugu yake na akasema, «Nitakuua.» Hābīl akajibu, «Kwa hakika Mwenyezi Mungu Huikubali sadaka itokayo kwa wale wenye kumuogopa.»
Hābīl akasema, akimpa mawaidha ndugu yake, «Iwapo utaunyosha mkono wako kwangu ili uniue, hutapata kutoka kwangu mfano wa kitendo chako. Mimi namuogopa Mwenyezi Mungu mola wa viumbe wote.
«Mimi nataka urudi ukiwa umebeba dhambi la kuniua mimi na dhambi lililokuwa juu yako kabala ya hilo, upate kuwa ni miongoni mwa watu wa Motoni na watakaosalia humo. Na hayo ndiyo malipo ya wanaofanya uadui.»
Qābīl alipomuua ndugu yake, hakujua aufanye nini mwili wake. Hapo Mwenyezi Mungu Alimtuma kunguru, akawa anafukuwa shimo katika ardhi ili amzike humo kunguru aliyekufa, ili amjulishe Qābīl namna ya kuuzika mwili wa ndugu yake. Qābīl alistaajabu na akasema, «Kwani nimeshindwa kufanya vile kunguru huyu alivyofanya nikapata kuificha aibu ya ndugu yangu?» Hapo Qābīl alimzika ndugu yake. Na baada ya hasara aliyorudi nayo, Mwenyezi Mungu alimpa mateso ya majuto.