Hayo masanamu yenu si chochote ila ni majina tu yasiyo na maana yoyote ya kiungu. Mmeyatunga nyinyi na baba zenu kwa kufuata pumbao lenu la upotovu. Mwenyezi Mungu hakuteremsha nayo hoja yoyote ya kusadikisha huo uzushi wenu mnao wadaia. Na hawa hawafuati ila ni dhana tu, na kipendacho nyoyo zao zilio potoka na kuacha maumbile yaliyo sawa. Na hakika yalikwisha wajia kutoka kwa Mola wao Mlezi yenye uwongofu, laiti wangeli ufuata huo!
Na malaika wengi wa mbinguni, juu ya ubora wa vyeo vyao, haufai kitu uombezi wao isipo kuwa baada ya kupewa idhini huyo mwombezi na Mwenyewe Mtukufu, na kumridhia huyo mwenye kuombewa.