Basi alipo kuja Isa a.s. akawaita watu wake wafuate Njia Iliyo Nyooka, wengi wao walikataa. Alipo yajua hayo aliwaelekea na kuwaambia: Ni nani atakaye nisaidia katika kazi hii niifanyayo ya kuitia kwenye Haki? Wakamjibu baadhi ya Waumini wenye kumuamini Mwenyezi Mungu na yeye: Sisi tunakuunga mkono, na tutakusaidia, kwa sababu wewe ni Mwitaji, unaita watu wende kwa Mwenyezi Mungu. Na shuhudia kuwa sisi tumemsafia Mwenyezi Mungu na ni wenye kufuata amri zake.