Ewe Muhammad! Waambie watu wako: Nimepata wahyi kwamba kikundi cha majini kimesikia kusoma kwangu Qur'ani, nao wakawaambia wenzao: Hakika sisi tumeisikia Qur'ani ya namna ya peke yake, hatujapata kusikia mfano wake kabla yake,
inaitia kwenye uwongofu na usawa. Kwa hivyo tumeiamini hiyo Qur'ani tuliyo isikia; na kabisa hatutamshirikisha Mola wetu Mlezi aliye tuumba na kutulea na chochote katika waja wake.
Na walikuwako wanaume katika wanaadamu wakitafuta ulinzi kwa wanaume wa kijini. Basi hao binaadamu hawakuwazidishia majini ila kuzidi uasi na ujinga na ujeuri.
Na hakika majini walidhani, kama mlivyo dhani nyinyi, enyi binaadamu, kwamba Mwenyezi Mungu hatamfufua yeyote baada ya kwisha kufa, wala hatowaletea watu Mtume yeyote wa kibinaadamu.
Na hakika sisi tulitaka kufikilia mbinguni, tukakuta kumejaa walinzi wa kimalaika wenye nguvu, na vimondo vinavyo unguza kutoka upande huo.
Na sisi kabla ya leo tulikuwa tukikaa pande za mbinguni kwenye makao kwa ajili ya kuchunguza khabari za mbinguni. Lakini sasa mwenye kutaka kusikiliza anakuta vimondo vinamngojea kumzuia na kumteketeza.
Na hakika sisi hatujui imekusudiwa adhabu kwa walioko katika ardhi kwa huku kulindwa mbingu hata ikazuiliwa kusikilizwa, au Mola wao Mlezi anawatakia kheri na uwongofu?
Na hakika miongoni mwetu wapo walio wema wachamngu, na miongoni mwetu pia wapo walio kinyume na hivyo. Na hao ni walio wastani katika wema wao. Kwa hivyo sisi ni wa makundi mbali mbali.
Na hakika sisi tumeyakinika kwamba hatutamshinda Mwenyezi Mungu popote tutapo kuwapo katika ardhi, wala hatutamshinda hata tukifanya tuikimbie hukumu yake kwendea mbinguni.
Na hakika sisi tulipo isikia Qur'ani tuliiamini. Na mwenye kumuamini Mola wake Mlezi basi hachelei kupunguziwa chochote katika mema yake, wala kudhulumiwa kwa kuzidishiwa maovu yake.
Na hakika kati yetu wapo Waislamu wenye kuikubali Haki, na miongoni mwetu wapo wenye kuiacha njia ya uwongofu. Basi wenye kusilimu hao wameifuata njia ya Haki, na ni wenye kufanya jitihada katika kuikhiari njia hiyo.
Na hakika lau kuwa watu na majini wakifuata Njia ya Uislamu, wala wasende upogo wakaiwacha, basi bila ya shaka tutawanywesha maji mengi yatakayo enea nyakati za haja.
Ili tuwajaribu tuwaone vipi watavyo mshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema anazo waneemesha. Na mwenye kukengeuka na ibada ya Mola wake Mlezi atamtia katika adhabu ya mashaka asiyo yaweza kuyachukua.
Na imefunuliwa kwangu kwamba kwa hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu peke yake. Basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu.
Na imefunuliwa kwangu kwamba alipo simama Mja wa Mwenyezi Mungu, Muhammad, katika Swala yake akimuabudu Mwenyezi Mungu, majini walijikusanya makundi kwa makundi, wakistaajabu kwa waliyo kuwa wakiyaona na wakiyasikia.
Sema: Hakika mimi hapana yeyote awezae kuniondolea adhabu nikimuasi Mwenyezi Mungu. Wala sipati pa kukimbilia, kuikimbia adhabu yake.
Lakini niliwezalo ni kufikisha Ujumbe wa Mwenyezi Mungu na Risala zake alizo nituma nizifikishe. Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na akaipuuza Dini ya Mwenyezi Mungu, basi hakika mtu huyo atapata Moto wa Jahannamu abakie humo milele.
Hata watakapo iona adhabu waliyo ahidiwaa, hapo basi watajua wakati itapo shuka, nani mwenye msaidizi dhaifu asiye na nguvu, na yupi mchache wa idadi. Ni wao au Waumini?
ila Mtume aliye mridhia kumjuvya baadhi ya hiyo siri. Naye humwekea mbele ya huyo Mtume na nyuma yake Malaika wa kumkinga na wasiwasi.
Ili Mwenyezi Mungu ayajue hayo yametokea kwa kuwafikiana na alivyo kadiria, ya kwamba Manabii hakika wamefikisha Risala za Mola wao Mlezi. Na kwa hakika Yeye kesha jua kwa kufananua yote waliyo nayo, na anajua idadi ya viumbe vyote. Hapana kitu kinacho mpotea Yeye.