Washirikina wa Kiarabu walikakamia katika inadi yao kumfanyia Muhammad, wakamtaka kama wale kaumu zilizo tangulia zilivyo wataka Manabii wao. Wakasema kuwa hawatomuamini ila Mwenyezi Mungu aseme nao, na awaletee ishara, au muujiza wa kuuona utakao onesha ukweli wake. Haya ni kama walivyo sema Wana wa Israili kumwambia Musa: Hatukuamini mpaka tumwone Mwenyezi Mungu na aseme nasi. Na kama masahaba (wanafunzi) wa Isa walipo mtaka awateremshie chakula kutoka mbinguni. Na haya yote ni kuwa nyoyo za makafiri na wapinzani wenye inda katika kila umma zimefanana. Haki haidhihiriki ila kwa wale ambao kuona kwao kumesafika, na akili zao zimeelekea kufuata Yakini, na kuitaka Haki.