Taluti alipo toka nao aliwaambia: "Mwenyezi Mungu anakujaribuni kwa mto ambao mtaukuta njiani mwenu. Msinywe katika mto huo ila tama moja tu. Mwenye kunywa zaidi ya hivyo basi hayumo katika jeshi letu, wala jamii yetu. Kwani amekuwa ameacha kumt'ii Mwenyezi Mungu. Wala asinifuate ila yule ambaye hakunywa ila tama moja tu." Hawakuweza kuvumilia jaribio hili, wakanywa maji mengi, ila wachache tu kati yao. Basi akafuatana na hichi kikundi kidogo akavuka nao mto. Walipoona wingi wa maadui wao walisema: "Hatutoweza hii leo kupigana na Jaluti na askari wake kwa wingi wao na uchache wetu." Baadhi yao wenye nyoyo madhbuti kwa kutaraji kwao malipo ya Mwenyezi Mungu watapo kutana naye, walisema: "Msiogope kitu! Mara nyingi wachache wenye kuamini huwashinda wengi walio makafiri. Subirini, kwani ushindi watapata wenye kusubiri."