Mwenyezi Mungu huzigeuza hali za usiku na mchana kwa urefu na ufupi, na kwa kuanzia na kumalizikia, kwa mizunguko ya falaki. Hakika katika hayo pana mazingatio kwa wenye akili zilio nzima zenye busara, na kwa njia hiyo wakamuamini Mwenyezi Mungu.
Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu. Na ndiye aliye anzisha kila kitu kwa kupenda kwake. Na akaumba kila kilicho hai kutokana na asili moja ya shirika, nayo ni maji. Na kwa hivyo kila kihai hakiachi kuwa na maji. Kisha zinawakhitalifisha khitilafu nyengine kwa namna, na uwezo, na sura, na kadhaalika. Katika wanyama wapo wanao tambaa kwa matumbo yao, kama samaki, na nyoka. Na wapo wanao kwenda kwa miguu miwili kama wanaadamu na ndege. Na wapo wanao kwenda kwa miguu mine kama mahayawani wengi wa kufugwa na wa mwituni. Mwenyezi Mungu huumba apendavyo kwa njia mbali mbali, kuonyesha uwezo wake na ujuzi wake. Kwani ni Mwenye kutaka atakacho, na Mwenye kukhitari apendacho. Na Yeye ni Muweza wa kila kitu. "Na Mwenyezi Mungu ameumba kila kinyama kutokana na maji. Wengine katika wao huenda kwa matumbo yao, na wengine huenda kwa miguu miwili, na wengine huenda kwa miguu mine. Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu." Maji katika Aya hii tukufu ni maji ya uzazi, yaani vinyama vinavyo toa manii. Na Aya hii si kama imetangulia msafara wa sayansi katika kubainisha kuzalikana mtu kutokana na tone la manii, kama ilivyo kuja katika kauli yake Aliye tukuka: "Hebu naajitazame mtu, ameummbwa kwa kitu gani? Ameumbwa kwa maji yatokayo kwa kuchupa." (Sura Att'ariq 5,6), bali imetangulia pia katika kubainisha kwamba kila kinyama kinacho kwenda kwenye ardhi kimeumbwa kwa njia ya kuzalikana na vinyama vya manii, na vinga khitalifiana hivyo vinyama vya manii na sifa zao katika kila namna mnamo hizo namna za vinyama. Katika maana za kisayansi ambazo zaweza kuwa nazo hii Aya ni kuwa maji ni msingi wa kila kiumbe kilicho hai. Kwa mfano mwili wa mtu umekusanya 70% ya uzito wake kuwa ni maji. Yaani mtu mwenye uzito wa kilo 70, kiasi kilo 50 ni maji. Na kabla ya kuteremka Qur'ani haya hayakuwa yakijuulikana kabisa ya kuwa mtu ana sehemu hii kubwa ya mwili wake kuwa ni maji. Na maji ndio chakula cha dharura kabisa kwa mwanaadamu. Kwani hali mtu yamkini aishi siku 60 bila ya kula chakula chochote, hawezi kuishi bila ya maji kwa zaidi kuliko siku 3 mpaka 10 mwisho wake. Na maji ndio msingi wa kufanyika damu, na maji ya limfo, na ya katika ubongo wa mifupa, vimwagavyo na mwili, kama mkojo, na jasho, na machozi, na mate, na nyongo, na maziwa, na maji yanayo patikana katika viungo, na ambayo ndiyo sababu ya ulaini wa mwili. Na yakikosekana 20% ya maji yake basi mwanaadamu hukabiliwa na mauti. Na maji huyayusha vyakula vikasahilika kufyonzeka. Na kadhaalika huyayusha makombo yenye asili ya vilivyo hai au maadini katika mkojo na jasho. Na kwa namna hii maji yana sehemu kubwa zaidi na muhimu kabisa katika kuumbwa kwa mwili. Na kwa hivyo yamkini kusema kwamba kila kiumbe kilicho hai kimeumbwa kutokana na maji.
Na hakika Sisi tumeteremsha kwa wahyi Aya zilizo wazi za kubainisha hukumu na mawaidha, na zinazo piga mifano. Na Mwenyezi Mungu humwezesha kwenye kheri ampendaye katika waja wake ambao wapo tayari kuziangalia na kufaidika nazo.
Na wanaafiki husema kwa ndimi zao: Tumemuamini Mwenyezi Mungu na Mtume, na tunazifuata amri zao. Na wanapo tiwa mtihanini kikundi kati yao hukataa kushirikiana na Waislamu katika kazi ya kheri, kama Jihadi na nyenginezo, baada ya kauli yao hii. Na watu hawa si Waumini wa kweli, wala hawastahiki kutumiliwa jina la Waumini kwao.
Na katika hali zao ni kuwa wakitakiwa kuhukumiwa mbele ya Mtume kwa jambo alilo literemsha Mwenyezi Mungu, unaafiki wa baadhi yao hudhihiri, na wao hukataa kuhukumiwa wakijua kuwa haki ni ya wale makhasimu zao.
Na kwa nini wanasimama msimamo huu katika kushitakiana mbele ya Mtume? Ni kwa sababu nafsi zao zimesibiwa na maradhi ya upofu, na kwa hivyo haziridhiki na hukumu yako ya haki? Au ni kwa kuwa wao wanatilia shaka uadilifu wa Muhammad s.a.w. katika kuhukumu? Si lolote katika hayo kabisa. Lakini hao ni madhaalimu walio dhulumu nafsi zao na wengineo kwa sababu ya ukafiri wao na unaafiki wao na kuiacha kwao haki.
Hakika kauli ya haki ifaayo kwa Waumini wa kweli wanapo itwa wahukumiwe kwa mujibu wa yaliyo kuja kutoka kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ni kuwa waseme kwa kukubali na kunyenyekea: Tumesikia wito wako, ewe Muhammad! Na tumeridhia hukumu yako. Na hao ndio watao kuwa watu wa kufanikiwa katika dunia yao na Akhera yao.
Na wenye kumt'ii Mwenyezi Mungu na kuridhia anayo yaamrisha Mtume s.a.w. na wakaiogopa dhati ya Mwenyezi Mungu Tukufu, na wakaukumbuka Utukufu wake, na wakaikhofu ghadhabu yake, hao ndio watakao pata radhi ya Mwenyezi Mungu na mapenzi yake, na neema za Pepo, na ndio wenye kupata kheri tupu.
Na wanaafiki wanaapa kwa ukomo wa nguvu za viapo vyao, kwamba wewe, Muhammad, ukiwaamrisha watoke nawe kwenda vitani watakut'ii. Waambie: Msiape! Kwani mambo yatakikanayo kwenu mnayajua, hapana hata mmoja wenu asiye yajua. Wala yamini zenu za uwongo haziondoi ujuzi huo. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua baraabara kila linalo tokana nanyi, na Yeye atakulipeni kwayo.