Na saidieni katika kujitenga na zina na yanayo pelekea zina, kwa kuwaoza ambao bado hawajaoana miongoni mwa wanaume wenu na wanawake wenu, na walio kuwa wanafaa kwa hayo katika watumwa wenu. Na wala umasikini usiwe sababu ya kuzuilia kuoa. Kwani Mwenyezi Mungu atasahilisha njia za maisha mazuri kwa mwenye kutaka kuishi maisha safi. Na fadhila za Mwenyezi Mungu ni kunjufu, na Yeye anajua kabisa niya za watu, na kila lipitalo katika ulimwengu.
Na ambao hawakupata uwezo wa fedha za kuolea basi wafuate mojapo wa njia nyengine kama saumu na riyadha na kazi za kutumia akili . Kwa hayo hujikurupusha mpaka Mwenyezi Mungu akawafungulia kwa fadhila zake zitakazo wawezesha kuoa. Na watumwa ambao wanataka kuandikiana nanyi ili wapate uhuru wao ni waajibu juu yenu kuwakubalia walitakalo, mkijua kuwa watatimiza kutekeleza na wanaweza. Na juu yenu kuwasaidia waweze kutimiza walio andikiana nanyi, na hayo ama ni kwa kuwapunguzia shuruti mlizo andikiana nao, au kwa kuwapa mali katika mali aliyo kuneemesheni Mwenyezi Mungu, mkawapa katika Zaka au Sadaka. Na ni haramu juu yenu kuwafanya vijakazi vyenu njia ya pato la duniani rakhisi kwa kuwafanya makahaba, na mkawalazimisha kwa hayo. Na vipi mnakwenda kumlazimisha uchafu anaye taka kuwa safi? Na mwenye kuwalazimisha, basi Mwenyezi Mungu humsamehe mwenye kulazimisha pindi akitubu kwa dhambi zake za kulazimisha. Kwani hakika Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu wa maghfira na rehema. Haya yanaelezwa na kauli ya Mtume s.a.w.: "Enyi vijana! mwenye kuweza kuwoa na aoe kwani hivyo linalindwa jicho, unahifadhiwa utupu. Asiye weza na afunge, kwani hivyo ni kinga yake."
Na Sisi tumekuteremshieni katika Sura hii na nyenginezo Aya zilizo wazi zenye kubainisha hukumu. Na tumekuteremshieni mifano ya hali mbali mbali za walio tangulia, na uwongozi, na mawaidha ambayo kwayo watapata faida wenye kumkhofu Mwenyezi Mungu.
Mwenyezi Mungu ndiye chanzo cha Nuru ya katika mbingu na ardhi. Yeye ndiye Mwenye kunawirisha vyote hivyo kwa nuru yote tunayo iona na tukenda ndani yake, na ya maana, kama Nuru ya Haki na uadilifu, na ilimu, na fadhila, na uwongofu, na Imani, na kwa ushahidi na athari kama alivyo waahidi viumbe vyake, na kwa vyote vinavyo onyesha kuwepo kwa Mwenyezi Mungu, na vikalingania Imani kumuamini Yeye Subhanahu. Na mfano wa Nuru yake Tukufu na dalili zake zilizo zagaa kwa uwazi ni kama mfano wa Nuru ya taa yenye kung'aa kwa ukali kabisa, iliyo wekwa kwenye shubaka la ukutani ili kuukusanya mwangaza wake na kuzidi kuupa nguvu. Na taa hiyo imevikwa tungi la kigae safi linameremeta kama inavyo meremeta nyota. Na taa ile inawaka kwa mafuta ya mti wenye baraka nyingi, ulio pandwa kwenye udongo mzuri na pahali pazuri. Mti huu ni mzaituni unao mea pahala pa kati na kati. Basi huo si wa mashariki ukakosa joto la jua wakati wa alasiri, wala si wa magharibi ukakosa joto la jua wakati wa asubuhi. Bali huo uko juu ya kilele cha mlima, au katika uwazi wa ardhi unao patisha jua mchana kutwa. Mafuta ya mti huu yanakaribia kutoa mwanga kwa ubora wa usafi wake hata ikiwa hayajaguswa na moto wa taa. Mambo haya yote yanazidisha mwangaza wa hiyo taa juu ya mwangaza wake, na Nuru juu ya Nuru. Na namna hii ndio zinakuwa dalili zilizo enea katika ulimwengu, za kuonekana na kupimika kwa akili; ni Ishara zilizo wazi hazitaki kutiliwa shaka yoyote kwa kuwepo Mwenyezi Mungu, na kuwajibikia Imani kumuamini Yeye, na Risala za Mitume aliyo waleta. Na Mwenyezi Mungu humwezesha kufikia Imani amtakaye kwa njia ya dalili hizi ikiwa huyo mtu atajaribu kunafiika na nuru ya akili yake. Na Mwenyezi Mungu ameleta mifano ya kuweza kuhisiwa na kuonekana ili iwe wepesi kuelewa mambo ya kiakili. Na Yeye Subhanahu ni Mkunjufu wa ujuzi, anawajua wenye kuangalia Ishara zake na wenye kuzipuuza na wakapanda kiburi. Naye atawalipa kwa hayo.
Hakika wapo watu wanao mtakasa Mwenyezi Mungu na wanamuabudu misikitini ambayo Mwenyezi Mungu ameamrisha ijengwe na iamirishwe kwa kudhukuriwa Mwenyezi Mungu, nao wameshughulikia hayo asubuhi na jioni.