Katika mitindo ya watu ni kuwa pale tunapo waneemesha baada ya kwisha patwa na shida katika nafsi zao, au ahli zao (watu wao), au mali zao, hawamshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema anazo waneemesha na kuwaondolea madhara. Bali huyakaabili hayo kwa kukakamia katika kuzikadhibisha na kuzikataa Ishara za Mwenyezi Mungu! Ewe Mtume! Sema: Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kukuhilikini na kukuadhibuni upesi upesi, lau kuwa si hukumu yake tangu hapo kukupeni muhula mpaka siku ya miadi aliyo iweka mwenyewe kwa ilimu yake peke yake. Hakika Wajumbe wetu, Malaika waliyo wakilishwa juu yenu wanaviandika vitimbi mnavyo vipanga, na Yeye Mwenyezi Mungu atakuhisabieni na atakulipeni.