Lakini tabia ya Firauni na wasaidizi wake ni kuto thibiti juu ya Haki. Wepesi kurejea kwenye khiana na uasi. Hao ni watu wa kigeugeu! Ikiwajia kutononoka na neema - na mara nyingi huwa hivyo - wao wakisema: Sisi tunastahiki haya tuliyo nayo kuwapita watu wengineo! Na likiwasibu la kuwaudhi, kama ukame, au tauni, au msiba wa miili au riziki, wakiona yamewapata hayo kwa ukorofi wa Musa na walio pamoja naye. Na wanaghafilika kuwa dhulma zao, na fisadi zao ndizo zilizo pelekea kuja hayo yanayo wapata! Basi na watanabahi, na wajue kuwa ujuzi wa ukorofi wao uko kwa Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye anaye wapatiliza kwa sababu ya vitendo vyao viovu. Yeye ndiye anaye wapelekea hayo yanao waudhi, wala si Musa na alio nao. Lakini wengi wao hawaijui Hakika ambayo haina shaka.