Katika yanayo dhihirisha uadui wa wao kwa wao na uadui wao wote kwa Waislamu, ni kule baadhi ya mataifa yao yalivyo kuwa yakiharibu pahala mwa ibada ya mataifa mengineo, na vile wale washirikina walivyo kuwa wakiwazuia Waislamu wasiingie Msikiti Mtakatifu wa Makka. Na hapana kabisa mwenye kudhulumu zaidi kuliko azuiaye asitajwe Mwenyezi Mungu katika pahala pa ibada, na akafanya juhudi kutaka kupaharibu. Watu hao watapata hizaya duniani, na Akhera watapata adhabu kubwa. Haiwafalii wao kufanya ukhalifu kama huu muovu, bali iwapasavyo ni kulinda utakatifu wa pahala pa ibada, wala wasiingie humo ila kwa unyenyekevu na kukhofu, wala wasizuilie kutajwa jina la Mwenyezi Mungu ndani yake. (Na ufisadi kama huu, bali ni mkubwa zaidi, ni wa wale wanao ghusubu (kuiba) mali za wakfu ya misikiti.)