Watu wa Peponi watawanadia watu wa Motoni kwa kuwaambia: Sisi tumekwisha ona thawabu alizo tuahidi Mola Mlezi wetu kuwa ni kweli. Je, nyinyi hiyo adhabu aliyo kuahidini Mola Mlezi wenu mmeiona kuwa ni kweli? Nao watajibu: Naam, Ndiyo! Basi mtangazaji atawatangazia watu wa Peponi na watu wa Motoni: Laana, yaani kunyimwa na kufukuzwa kwenye rehema ya Mwenyezi Mungu, ndio malipo ya wenye kuzidhulumu nafsi zao kwa ukafiri na upotovu.