[1] Huu ni mfano wa yule aliyekuwa katika giza kubwa, kwa hivyo akauwasha moto kutoka kwa mtu mwingine. (Tafsir Assa'dii) Na nuru ya moto huo ilitoka kwa Waislamu ambao wao (wanafiki) wanaishi pamoja nao. Na hakusema: Mwenyezi Mungu aliuondoa 'mwangaza wao'. Kwa sababu mwangaza ni ziada juu ya nuru. Kwa hivyo, aliondoa asili (nuru) na ziada yake (mwangaza). (Tafsir Ibn Al-Qayyim)
[1] Ni viziwi kwa sababu hawaisikii heri. Ni mabubu kwa sababu hawaitamki heri. Na ni vipofu kwa sababu hawaioni haki. Kwa hivyo, hawatarejea kwa haki kwa kuwa waliiacha baada ya kuijua. Tofauti na mwenye kuiacha haki kwa ujinga na upotovu, yeye yuko karibu zaidi na kurudi katika haki. (Tafsir Assa'dii)
[1] Hapa Mwenyezi Mugnu aliufananisha uwongofu aliowaongoza kwao waja wake, na mvua. Kwa sababu, nyoyo huhuishwa kwa uwongofu, kama vile ardhi huhuishwa na mvua. Na fungu la wanafiki katika uwongofu huo ni kama fungu la yule ambaye hakupata katika mvua isipokuwa giza, radi na umeme, wala hana fungu zaidi ya hayo katika yale yaliyokusudiwa kutoka kwa mvua hiyo kama vile uhai wa nchi, watu, miti na wanyama. (Tafsir Ibn Al-Qayyim)
[1] Aya imemalizika kwa kusema: "Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu." Kwa sababu aliwaonya wanafiki juu ya adhabu yake na uwezo wake, na akawaambia kwamba amewazunguka, na kwamba ana uwezo wa kuondoa kusikia na kuona kwao. (Tafsir Ibn Kathir)
[1] "Enyi watu" inawaamrisha wanadamu wote. (Tafsir Ibn Al-Qayyim)
[1] Unaonaje mtu ambaye atazinduka kutoka usingizini au katika hali ya kughafilika, (yani kuumbwa) na akakuta ametandikiwa zulia zuri (yani ardhi) na ameekewa hema (yani mbingu) hapo; na kuwekewa chakula na kinywaji. Je hapaswi kumshukuru aliyetenda haya? Basi hii ndiyo maana ya aya hii. (Tafsir Al-Baqqaa'ii)
[2] "Na hali nyinyi mnajua" kwamba, Mwenyezi Mungu peke yake ndiye aliyefanya vitendo hivyo vyote. Basi ni vipi mnamfanyia washirika? (Tafsir Ibn Al-Qayyim)