Ewe Nabii! Lau kuwa Mola wako Mlezi angeli penda angeli wafanya watu wote wafuate Dini moja, wakimt'ii Mwenyezi Mungu kwa ut'iifu wa maumbile, kama Malaika. Na ulimwengu ungeli kuwa sio ulimwengu huu. Lakini Yeye Subhanahu hakutaka hayo, bali amewaacha waweze kuchagua wenyewe. Basi hawaachi kukhitalifiana katika kila kitu, hata katika misingi ya imani, kama kumuamini Mwenyezi Mungu, na Malaika wake, na Vitabu vyake, na Mitume wake, na Siku ya Mwisho - mambo ambayo haifai kukhitalifiana kwayo. Wao hufuata nyoyo zao, na matamanio yao, na fikra zao, kila kikundi kimeshikilia kwa nguvu rai ile ile walio kutana nayo kwa baba zao!