Hayo hutokea ili mwisho wao huwa kuikanya fadhila yetu kwa yale tuliyo wapa. Basi enyi makafiri! Stareheni na hayo msiyo yatolea Haki ya shukrani. Mtakuja kuujua mwisho wa ukafiri!
Na washirikina huyapa masanamu yao, ambayo wanayaita kwa ujinga wao kuwa ni miungu, sehemu ya kujikaribisha kwayo kutokana na zile riziki tulizo wapa Sisi, katika makulima na mifugo na vyenginevyo. Nakuulizeni, kwa Utukufu wangu, enyi washirikina, hayo mliyo khitalifiana kwayo katika uwongo wenu na upotovu mlio uzua. Na Mimi nitakulipeni kwayo.
Na hujaalia kumpa Mwenyezi Mungu yale wayachukiayo wao, kwa kudai kuwa Malaika ni watoto wake wa kike, na wao wanawaabudu. Mwenyezi Mungu apishe mbali na hayo! Na wao ati wanajipa wayapendayo nayo ni watoto wanaume.
Anajaribu kujificha watu wasiione huzuni ya machungu yaliyo mpata kwa kupewa khabari ya binti aliye zaliwa. Anatapatapa: amwache hai juu ya fedheha anayo iona, kama anavyo jigamba? Au amzike katika udongo naye yuhai mpaka afe? Ewe msikilizaji! Zingatia uwovu wa vitendo vya watu hawa! Na uovu gani wa kumhukumia Mwenyezi Mungu mabinti ambao wao wanawachukia!
Ni hali mbaya ya wasio amini Akhera na yote yaliyoko huko ya thawabu na adhabu, nayo ni ile haja ya kutaka watoto wa kiume na kuchukia watoto wa kike. Na Mwenyezi Mungu ana sifa tukufu. Yeye ni Mkwasi, hahitajii kitu, wala hana haja ya mtoto. Naye ni Mwenye kushinda, Mwenye nguvu, wala hana haja ya msaidizi.
Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angeli fanya haraka kuwaadhibu watu kwa dhulma zao wanazo zifanya, basi asingeli mwacha hata mnyama mmoja juu ya ardhi. Lakini Yeye kwa upole wake na hikima yake anawaakhirisha madhaalimu mpaka wakati aliyo uweka, nao ndio wakati utapo kwisha muda wao. Ukija wakati huo hawato taakhari hata kidogo, wala hawato tangulia.
Na washirikina wanamnasibisha Mwenyezi Mungu mabinti na ushirika mambo ambayo wao wanayachukia. Na ndimi zao zinatamka uwongo wanapo dai ya kwamba, kama walivyo kuwa na utajiri na utawala duniani, basi kadhaalika Akhera nao watapata malipo mema kwa Mwenyezi Mungu watapo fufuliwa; nayo ni Pepo! Hapana shaka hao watatiwa Motoni, nao watasukumwa huko kabla ya wengineo.
Ewe Nabii! Jua kwa yakini kwamba Sisi tuliwatuma Mitume kabla yako kwa kaumu nyingi kama tulivyo kutuma wewe kwa watu wote. Lakini Shetani aliwapambia ukafiri, na ushirikina, na maasi. Basi wakawakanya Mitume wao, na wakawaasi, na wakamsadiki Shetani na wakamt'ii yeye. Basi yeye amekuwa ndiye mwenye kuyatawala mambo yao katika dunia, akiwapambia mambo ya kuwadhuru. Na Akhera watapata adhabu yenye machungu makali.
Na hatukukuteremshia wewe hii Qur'ani isipo kuwa upate kuwabainishia watu haki katika yale waliokhitalifiana kwayo katika dini, na ili ipate kuwa ni uwongofu ulio timia na rehema ilio enea kwa kaumu yenye kumuamini Mwenyezi Mungu na Kitabu alicho kiteremsha.