Kwa Mwenyezi Mungu peke yake ndio unarejea ujuzi wa kusimama Saa ya Kiyama. Matunda hayatoki kwenye vifuniko vyake, wala mwanamke hachukui mimba wala hazai ila awe Yeye anajua. Na kumbuka siku ambayo Mwenyezi Mungu atawaita washirikina, kwa kuwakebehi, awaambie: Wako wapi hao washirika wangu mlio kuwa mkiwaomba badala yangu? Watasema kwa kutaadhari: Ewe Mwenyezi Mungu! Tunakujuvya kuwa sisi hatuna wa kushuhudia kuwa wewe una mshirika yeyote.
Na hao miungu ya ushirikina walio kuwa wakiwaabudu watawapotea, na waliyakinika kuwa hawana pa kukimbilia.
Mwanaadamu hachoki kumwomba Mola wake Mlezi kwa kheri za kidunia. Ikimpata shari basi huwa mwingi wa kuikatia tamaa kheri, na kuvunjika moyo hadi, ya kwamba Mwenyezi Mungu hamwitikii dua yake.
Tunaapa: Tukimwonjesha mtu neema, kwa fadhila yetu, baada ya dhara kubwa iliyo msibu bila ya shaka husema: Hii neema niliyo ipata ni haki yangu mimi. Wala sidhani kuwa Kiyama kitakuja. Na ninaapa ikitokea nikarejeshwa kwa Mola wangu Mlezi basi na huko kwake bila ya shaka nitapata malipo mema. Lakini Sisi tunaapa: Hapana shaka tutawalipa walio kufuru, Siku ya Kiyama, kwa vitendo vyao! Na hapana shaka tutawaonjesha adhabu kali iliyo rindikwa juu kwa juu!
Na tukimneemesha mtu huacha kutushukuru, na akajitenga mbali na Dini yetu. Na tukimwonjesha shari basi huwa mwingi wa kuomba madua.
Ewe Muhammad! Waambie: Hebu nambieni; ikiwa hii Qur'ani imetoka kwa Mwenyezi Mungu nanyi mkawa mnaikataa, basi nani aliye kuwa mbali mno na Ukweli kuliko huyo aliye kinyume na Haki?
Karibuni hivi tutawaonyesha hao wanao zikataa Ishara zetu zenye kuonyesha ukweli wako katika pande za mbinguni na ardhi, na katika nafsi zao wenyewe, mpaka yawadhihirikie ya kwamba uliyo waletea ni Haki tupu si vinginevyo. Je! Wanakataa kuwa Sisi tunawaletea Ishara hizo? Je! Haitoshi kuwa Mola wako Mlezi ni Mwenye kukizunguka kila kitu?
Ama hakika hawa makafiri wamo katika shaka kubwa kukutana na Mola wao Mlezi, kwa sababu ya kuwa hawaamini kufufuliwa. Ama hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kukizunguka kila kitu kwa ujuzi wake na uweza wake.