Mwenyezi Mungu ndiye anaye stahiki kuabudiwa pekee. Yeye ndiye Mwenye kubaki, Mwenye kuyasimamia mambo ya viumbe daima. Haghafiliki kabisa, wala hanyong'onyei, wala halali wala yanayo fanana na hayo, kwani Yeye hasifiki na upungufu wa chochote. Yeye pekee ndiye Mwenye kumiliki mbingu na ardhi, wala hana mshirika yeyote katika hayo. Kwa hivyo hapana kiumbe anaye weza kumwombea mwenginewe ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Yeye Subhanahu wa Taa'la anajua kila kitu. Anayajua yaliyo kuwa na yatayo kuwa. Hapana mtu anaye weza kujua kitu katika ilimu ya Mwenyezi Mungu ila atakavyo Yeye ajue na aridhie. Utawala wake umeenea mbinguni na ardhini. Hayamhangaishi Yeye kuyadabiri hayo, kwani Yeye ametukuka, hana upungufu wala kushindwa na jambo, Muadhamu katika utukufu wake na utawala wake. Katika haya upo ushahidi wa kuonyesha ujuzi wa Mwenyezi Mungu wa daima, na Kusimamia kwake kusio koma kwa yote ya mbinguni na duniani. Pia pana ishara ya kuwa Mwenyezi Mungu hapitikiwi na vituko vinavyo zuka.Ilimu ya Sayansi imethibitisha kuwa kulala ni katika sifa ya wanyama na mimea iliyo hai. Ikiwa Mwenyezi Mungu halali basi Yeye ni hai kwa uhai ulio elekeana na dhati yake, lakini sio kama vilivyo hai vinginevyo.