Na zipo dalili nyingi na Ishara kwa kila mwenye akili juu ya kuwapo kwake na Ungu wake. Miongoni mwa hizo ni hizi mbingu mzionazo zinazo pitiwa na sayari kwa nidhamu bila ya kuzahamiana wala kugongana, zikiuletea ulimwengu huu joto na nuru. Na pia hii dunia yenye bara na bahari, na kupishana usiku na mchana, pamoja na manufaa yake. Katika Ishara na dalili hizo ni kuzingatia marikebu zipitazo baharini zikibeba watu na vifao vyao, na hapana aziendeshao hizo ila Mwenyezi Mungu. Ni Yeye ndiye anaye zituma pepo zinazo leta mvua. Na mvua ikateremka ikahuisha wanyama na ikanywesha ardhi na mimea. Na hizo pepo kwa mivumo yake ya kila namna, na mawingu yaliyo tundikwa baina ya mbingu na ardhi: Jee, yote haya yamesimama kwa uangalifu namna hii na kwa hukumu kama hizi wenyewe tu? Au vimeundwa na Mwenye Kujua Mwenye Uwezo?