Enyi Waumini! Msipoteze thawabu za sadaka zenu kwa kudhihirisha kuwa mnawafadhili wenye haja na kuwaudhi. Hivyo mnakuwa kama wale wanao toa mali zao kwa ajili ya kutafuta umaarufu na kupenda wasifiwe na watu., nao hata hawamuamini Mwenyezi Mungu wala Siku ya Mwisho. Hali ya mwenye kuonyesha kutoa kwake ni hali ya jiwe manga lenye udongo. Likateremkiwa na mvua kubwa, udongo wote ukaondoka. Basi kama mvua kubwa inavyo chukua udongo wenye mbolea likabaki jiwe tupu, basi kadhaalika masimbulizi, na maudhi, na kuonyesha watu huharibu thawabu za sadaka. Hayo hayamnufaishi mtu, na hizo ni sifa za makafiri. Epukaneni nazo! Kwani Mwenyezi Mungu hawawafikishi makafiri kupata kheri na uwongozi mwema.