Kama Mwenyezi Mungu alivyo anzisha uumbaji wa viumbe peke yake, basi marejeo yenu, na marejeo ya viumbe vyote ni kwake Yeye. Na Mwenyezi Mungu ameahidi hivyo kwa ahadi ya kweli isiyo na khitilafu. Na hakika Yeye Subhanahu ameanzisha kuumba viumbe kwa kudra yake, na vitapo teketea atavirejesha kwa kudra yake, ili awalipe Waumini wenye kumt'ii thawabu kwa uadilifu ulio timia. Ama makafiri, wao huko katika Jahannamu watapewa vinywaji vinavyo tokota kweli kweli, na watapata adhabu yenye kutia machungu kuwa ni malipo ya ukafiri wao.