Ewe Muhammad! Waambie watu wako: Nimepata wahyi kwamba kikundi cha majini kimesikia kusoma kwangu Qur'ani, nao wakawaambia wenzao: Hakika sisi tumeisikia Qur'ani ya namna ya peke yake, hatujapata kusikia mfano wake kabla yake,
inaitia kwenye uwongofu na usawa. Kwa hivyo tumeiamini hiyo Qur'ani tuliyo isikia; na kabisa hatutamshirikisha Mola wetu Mlezi aliye tuumba na kutulea na chochote katika waja wake.
Na walikuwako wanaume katika wanaadamu wakitafuta ulinzi kwa wanaume wa kijini. Basi hao binaadamu hawakuwazidishia majini ila kuzidi uasi na ujinga na ujeuri.
Na hakika majini walidhani, kama mlivyo dhani nyinyi, enyi binaadamu, kwamba Mwenyezi Mungu hatamfufua yeyote baada ya kwisha kufa, wala hatowaletea watu Mtume yeyote wa kibinaadamu.
Na hakika sisi tulitaka kufikilia mbinguni, tukakuta kumejaa walinzi wa kimalaika wenye nguvu, na vimondo vinavyo unguza kutoka upande huo.
Na sisi kabla ya leo tulikuwa tukikaa pande za mbinguni kwenye makao kwa ajili ya kuchunguza khabari za mbinguni. Lakini sasa mwenye kutaka kusikiliza anakuta vimondo vinamngojea kumzuia na kumteketeza.
Na hakika sisi hatujui imekusudiwa adhabu kwa walioko katika ardhi kwa huku kulindwa mbingu hata ikazuiliwa kusikilizwa, au Mola wao Mlezi anawatakia kheri na uwongofu?
Na hakika miongoni mwetu wapo walio wema wachamngu, na miongoni mwetu pia wapo walio kinyume na hivyo. Na hao ni walio wastani katika wema wao. Kwa hivyo sisi ni wa makundi mbali mbali.
Na hakika sisi tumeyakinika kwamba hatutamshinda Mwenyezi Mungu popote tutapo kuwapo katika ardhi, wala hatutamshinda hata tukifanya tuikimbie hukumu yake kwendea mbinguni.
Na hakika sisi tulipo isikia Qur'ani tuliiamini. Na mwenye kumuamini Mola wake Mlezi basi hachelei kupunguziwa chochote katika mema yake, wala kudhulumiwa kwa kuzidishiwa maovu yake.