Watu wamekithirisha maneno juu ya Kibla kama kwamba wema wote ni hayo tu. Hivi sivyo. Kuelekea upande fulani, mashariki au magharibi, sio msingi wa Dini na kupata kheri, lakini kupata wema ni mambo kadhaa wa kadhaa, baadhi yake ni nguzo za itikadi sahihi, na baadhi yake ni katika misingi ya tabia njema na ibada. La kwanza: kumuamini Mwenyezi Mungu, na Siku ya kufufuliwa na kukusanywa na kuhisabiwa na yatakayo tokea Siku ya Kiyama; na kuamini Malaika, na Vitabu vilivyo teremka kwa Manabii, na kuwaamini wenyewe Manabii. Na pili: kutoa mali kwa kupenda na kuridhia nafsi kuwapa mafakiri katika jamaa, na mayatima, na wenye shida ya haja, na wasafiri walio katikiwa safari yao wasipate cha kuwafikishia wendako, na walio lazimika kuomba kwa haja walio nayo, na kukomboa watumwa. ( Walio fungwa na kutawaliwa na dhaalimu ni watumwa pia. )Tatu: kushika Swala. Lane: kutoa Zaka iliyo lazimishwa. La tano: kutimiza ahadi bilhali wal maal. La sita: kustahamili maudhi yanayo teremkia roho na mali, mnapo pambana na adui zama za vita. Basi wenye kukusanya imani hizi na vitendo hivi vya kheri ndio walio sadikisha Imani yao, na wao ndio wanao jilinda na ukafiri na mambo machafu na wakayaepuka.